Humphrey Polepole
Rasimu ya Warioba iliwapa wapiga kura uwezo wa kuwawajibisha wabunge kwa  kupiga kura ya kutokuwa na imani nao wakati wowote kama wakienda kinyume na masilahi ya wananchi katika jimbo husika. Wananchi walijiuliza kama mbunge ni mtumishi wao, iweje hayuko katika kituo cha kazi kwa miezi kadhaa na wasiweze kumwajibisha mpaka miaka mitano?
Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya.

1. Kupunguzwa kwa madaraka ya raisi

Wananchi walipendekeza madaraka makubwa ya Rais hasa ya uteuzi yapunguzwe na ziundwe taasisi za kikatiba za kumshauri rais kabla hajafanya teuzi. Wananchi walipendekeza pia baada ya rais kumteua kiongozi basi itabidi mteuliwa huyo Bunge limthibitishe.
Katiba Inayopendekezwa imeyafuta haya yote na imemwongezea Rais madaraka.

2. Kutenganisha mamlaka ya mihimili ya dola

Wananchi walipendekeza uhuru zaidi kwa Bunge na mamlaka zaidi kwa Bunge kuisimamia, kuiwajibisha na kuishauri Serikali. Pendekezo hili linaenda sambamba na kutenganisha Serikali na Bunge, hali ambayo iko sasa. Rasimu ya Warioba ililipa Bunge mamlaka zaidi kuisimamia Serikali na hata pale ambapo Bunge lingekataa bajeti au muswada mbaya wa Serikali mara kadhaa, rais asingeliweza kulivunja Bunge. Wananchi walisema sana mawaziri wasitokane na wabunge, ili wabunge wafanye kazi ya uwakilishi pekee na mawaziri watumie weledi wao kumsaidia rais kazi za Serikali.
Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya.

3. Kumwajibisha mbunge

Rasimu ya Warioba iliwapa wapiga kura uwezo wa kuwawajibisha wabunge kwa  kupiga kura ya kutokuwa na imani nao wakati wowote kama wakienda kinyume na masilahi ya wananchi katika jimbo husika. Wananchi walijiuliza kama mbunge ni mtumishi wao, iweje hayuko katika kituo cha kazi kwa miezi kadhaa na wasiweze kumwajibisha mpaka miaka mitano?
Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya.

4. Vyanzo vya mapato vya kuaminika

Kuwapo kwa vyanzo vya mapato vya Serikali ya Jamhuri ya Muungano vitakavyogharimia mambo ya Muungano ambayo yamepunguzwa kutoka 22 hadi 7 lilikuwa pendekezo ambalo hata taasisi za Serikali zilipendekeza. Katiba Inayopendekezwa imerudisha mapato ya Muungano kama Katiba ya Mwaka 1977 na kwa kufanya hivyo tumerudi kwenye mgogoro wa msingi, kuchukua kodi tatu, ushuru wa forodha, ushuru wa bidhaa na mapato kutoka Zanzibar ni kuiua Zanzibar na kuifanya ishindwe kumudu matumizi yake ya ndani kwa mambo yasiyo ya Muungano na vivyo hivyo kwa Tanganyika.

5.Muundo wa shirikisho lenye mamlaka kamili

Kwa miaka nenda rudi tumekuwa na kitendawili cha ni muundo gani wa Muungano Jamhuri yetu inao. Kitendawili hiki kimeelezwa na wengi akiwamo Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere. Rasimu ya Warioba iliweka kwa mara ya kwanza Muundo Jamhuri ya Muungano kuwa ni wa Shirikisho lenye Mamlaka Kamili, nchi moja na yenye Serikali tatu. Kilichoongezwa ni na Rasimu ya Warioba ilikuwa Bunge na Serikali ya Tanganyika na siyo nchi ya Tanganyika kama ambavyo wengi wameaminishwa hivyo. Katiba Inayopendekezwa imerejesha na kuudhoofisha zaidi muundo wa Serikali mbili, kwa kuifanya Tanganyika au Tanzania Bara kuwa ndiyo Jamhuri ya Muungano na Zanzibar kuwa na mamlaka zaidi kwa mambo yasiyo ya Muungano ikiwamo kujiunga na jumuiya za kimataifa.

6. Kupunguza ukubwa wa Serikali

Wananchi walionesha kutofurahishwa na ukubwa wa Serikali unaopelekea matumizi makubwa ya fedha za walipa kodi. Walipendekeza uwapo wa Serikali ya Muungano iliyo imara, yenye ufanisi na ndogo. Rasimu ya Warioba ilisema idadi ya mawaziri isizidi 15.
Katiba Inayopendekezwa inasema mawaziri wasizidi 40, pendekezo hili halina uhalisia kwa sababu Serikali ya Muungano itashughulika na mambo ya Muungano na mambo yasiyo ya Muungano ya Tanganyika/ Tanzania Bara na kuifanya kuwa kubwa zaidi na hivyo kuhitaji mawaziri zaidi ya 40, kiufupi pendekezo hili halitekelezeki.

7. Tume ya Uhusiano na Uratibu

Rasimu ya Warioba ililenga kuhakikisha kunakuwapo uhusiano mzuri, mawasiliano na uratibu wa serikali zote tatu chini ya Mamlaka ya Serikali ya Muungano na kupitia Tume ya Uhusiano na Uratibu. Bunge Maalumu lilishindwa kuelewa mantiki ya pendekezo hili na Katiba Inayopendekezwa imelivuruga kabisa, kutoka pendekezo la Warioba la “Tume ya Uhusiano na Uratibu wa Serikali” hadi “Tume ya Uratibu wa Mambo ya Muungano” katika Katiba Inayopendekezwa.

8.Kupunguza ukubwa wa Bunge

Wananchi walizungumzia pia ukubwa wa Bunge la Jamhuri ya Muungano na gharama zinazoambatana nalo na wakapendeza Bunge dogo na lenye ufanisi mkubwa. Warioba alisema idadi ya wabunge isizidi 75, Bunge Maalumu likasema wabunge wasipungue 340 na wasizidi 390.

9. Ukomo wa vipindi vya ubunge

Wananchi walizungumzia nafasi za ubunge kuhodhiwa na watu fulani kwa miaka nenda rudi na wakapendekeza ifike mahali kuwe na ukomo ili kuleta uwakilishi mpana na mabadiliko. Rasimu ya Warioba iliweka ukomo wa vipindi vya ubunge kuwa vitatu na kuwa na ukomo wa miaka 15 kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano. Bunge Maalumu na Katiba Inayopendekezwa wamefuta pendekezo hili.

10. Kuwapo kwa tunu za Taifa

Wananchi walipendekeza uwapo wa tunu za Taifa katika Katiba, tunu hizi ni pamoja na utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji na lugha ya Taifa. Raia wa Tanzania walikuwa na wajibu wa kuheshimu tunu hizi lakini Katiba Inayopendekezwa imezifuta tunu hizi.

11. Maadili na miiko ya viongozi

Wananchi walizungumza kuporomoka kwa kiasi kikubwa kwa maadili ya jamii, watumishi na viongozi wa umma, wengi wakisema Katiba iainishe maadili na miiko ya viongozi wa umma ambayo kwayo tutawawajibisha. Katiba Inayopendekezwa imesema maadili na miiko kwa viongozi (mathalan kutenganisha biashara na uongozi ili kuepusha mgongano wa masilahi), isiwamo kwenye Katiba bali ikawekwe kwenye sheria.
12. Masharti yasiyoweza kubadilishwa na Bunge
Rasimu ya Warioba iliweka masharti ya kuzuia Bunge kubadili baadhi ya masharti mahususi ya Katib, ibara ya 119 isipokuwa kwa ridhaa ya wananchi kupitia kura ya maoni (mathalan malengo makuu ya Taifa, haki za binadamu n.k. Pia, bahati mbaya tulisahau kuweka na Sura ya tatu juu ya maadili). Masharti yote ya Ibara hii yamefutwa isipokuwa Muundo wa Muungano na Uwapo wa Jamhuri ya Muungano.

13. Kuwapo kwa Tume Huru ya Uchaguzi

Wananchi walizungumza umuhimu wa kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi ambayo itakuwa na jukumu la kusimamia chaguzi za Jamhuri ya Muungano. Ilisisitizwa juu ya umuhimu wa  tume kugawa majimbo ya uchaguzi na kwamba mwenyekiti wa tume na makamu wake wathibitishwe na Bunge ili kuwapa uhalali wa kitaifa, pendekezo hili limefutwa na Katiba Inayopendekezwa.

14. Usawa wa 50:50 kati ya wanawake na wanaume

Kuwapo uwiano wa uwalikishi wa 50:50 kati ya wanawake na wanaume ni lazima kwa mazingira ya sasa. Uwiano kati ya wanawake na wanaume katika vyombo mbalimbali vya dola hasa vile vya kutunga sheria limeendelea kuwa tatizo nchini na lililokaa kwa muda mrefu.
Wananchi na hasa wanawake na baadhi ya wanaume walipendekeza uwiano ulio sawa katika kufikia fursa hasa ukizingatia wanawake ndiyo wazalishaji wakubwa. Rasimu ya Warioba ilipendekeza katika kila jimbo kutakuwa na wabunge wawili, wa kike na wa kiume, Katiba Inayopendekezwa imefutilia mbali pendekezo hili muhimu

15. Kuanzishwa kwa mgombea huru

Haki ya wananchi kushiriki shughuli za umma imekuwa ikizuiwa siku nyingi na kwamba ushiriki katika shughuli za umma kama kiongozi wa kuchaguliwa inapaswa kuwa haki ya msingi ya mwananchi yeyote yule. Rasimu ilitoa haki ya mgombea huru bila vikwazo, Katiba Inayopendekezwa imeweka masharti magumu ambayo hakuna mtu anayeweza kuyatimiza kirahisi, kitendo hiki siyo sawa.

16. Msaada wa kisheria kwa wananchi

Wananchi walieleza kutokuridhishwa kwao na huduma za msaada wa kisheria kwa wananchi wenye uhitaji huo na wakapenda huduma ya msaada wa kisheria liwe suala la kikatiba kwa mwananchi yeyote yule na serikali iwajibike kutoa huduma hiyo.
Katiba Inayopendekezwa imesema wananchi hawatakuwa na haki ya kudai huduma hii kokote nchini, hata mahakama hazitaweza kusikiliza mashauri ama Serikali imetoa haki hii au haikutoa haki hii rejea Ibara ya 21.

17. Uhuru wa Mkuu wa Jeshi la Polisi

Rasimu ya Warioba ilipendekeza Mkuu wa Jeshi la Polisi atekeleze kazi zake kwa uhuru, bila woga, upendeleo wala chuki na kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na sheria za nchi. Masharti haya yamefutwa na Katiba Inayopendekezwa.

18. Tume ya Utumishi wa Jeshi la Wananchi Tanzania

Tume ya Warioba ilipendekeza kuwapo kwa Tume ya Utumishi ya Jeshi la Ulinzi la
Wananchi wa Tanzania itakayokuwa na jukumu la kusimamia masuala yote ya utumishi katika Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya licha ya wapiganaji kupendekeza utaratibu wa kusimamia masilahi yao kikatiba.

19. Tume ya Utumishi wa Jeshi la Polisi

Kutakuwa na Tume ya Utumishi wa Jeshi la Polisi itakayokuwa na jukumu la kusimamia utumishi wa Jeshi la Polisi. Katika uajiri wa askari wa Jeshi la Polisi, Tume ya Utumishi wa Jeshi la Polisi itazingatia kanuni na misingi ya utumishi iliyoainishwa katika Katiba hii

Itaendelea wiki ijayo

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

SOCIALIZE

twitterfacebookgoogle plusemail

IN CASE YOU MISSED IT

FOR INSURANCE SERVICES CLICK HERE