Mathias Chikawe

Waziri wa Mambo ya ndani ni miongoni mwa wanachama maarufu wa CCM walioshindwa kupita katika kura za maoni. Mathias Chikawe, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi aliyekuwa akiwania kupitishwa tena kugombea tena ubunge wa Nachingwea.

Chikawe ambaye pia alishindwa katika kinyang’anyiro cha urais kupitia chama hicho, alidondoshwa na Hassan Masala aliyepata kura 6,494 akifuatiwa naye akipata 5,128.
Mbali ya Chikawe pia manaibu waziri wanne wameangushwa katika kura hizo. Hao ni Mahadhi Juma Maalim (Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), Perera Ame Silima (Mambo ya Ndani), Amos Makala (Maji) na Saning’o ole Telele (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi).

Mahadhi Juma Maalim

Mahadhi alianguka katika Jimbo la Paje, Zanzibar kwa kupata kura 1,785 huku Jaffar Sanya Jussa ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) Mkoa wa kusini akiibuka mshindi kwa kura 3,368.

Perera Ame Silima

Silima aliyepata kura 1,218 katika Jimbo la Chumbuni alibwagwa na mpinzani wake, Ussi Pondeza aliyepata kura 1,952.

Dkt. Milton Makongoro Mahanga ajiunga CHADEMA

Naibu Waziri wa Kazi na Ajira ambaye pia ni Mbunge wa CCM jimbo la Segerea anayemaliza muda wake, Dkt. Milton Makongoro Mahanga naye ameshindwa katika kura za maoni, na hatimae kutangaza kuhamia CHADEMA.

Dkt. Mahanga ametangaza uamuzi huo mbele ya waandishi wa habari akiwa nyumbani kwake Segerea mwisho, ambapo amesema ameamua kuachana na Chama cha Mapinduzi (CCM) na kujiunga na (CHADEMA) baada ya kushuhudia mbinu chafu zilizotumia na baadhi ya wagombea dhidi yake.

Amos Makala

Katika Jimbo la Mvomero, Suleiman Murad alishinda kwa kura 13,165 dhidi ya Makalla ambaye alikuwa anatetea jimbo hilo akipata 10,973. Ambaye yupo katika Wizara ya Maji.

Saning’o ole Telele

Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Ole Telele alipata kura 5, 126 huku William ole Nasha akiibuka mshindi kwa kura 23, 563 akifuatiwa na Elias Ngolisa aliyepata 11, 442 na Dk Eliamani Lalkaita 7,135. Matokeo hayo hayakujumlisha kura za matawi matano ambayo Katibu wa CCM Wilaya ya Ngorongoro, Elihudi Shemauya alisema hayawezi kubadili matokeo.

Abdul Mteketa

Katika jimbo la Kilombero: Mbunge wa jimbo hilo, Abdul Mteketa alianguka baada ya kushika nafasi ya tatu kwa kupata kura 2,646 nyuma ya Abubakar Assenga aliyepata kura 6,629 na Abdul Liana 3,999.

Muhammed Seif Khatib

Katika Jimbo la Uzini, Muhammed Seif Khatib ameshindwa baada ya kupata  kura 1,333 huku mpinzani wake Salum Mwinyi Rehani akiibuka kidedea kwa kura 1,521.
Wagombea wengine ni Steven Nyoni (1,438), Amandus Chinguile (1,274), Fadhili Liwaka (1,171), Benito Ng’itu (797), Greyson Francis (671), Albert Mnali (763), Issa Mkalinga (466), Mustafa Malibiche (427) na Ali Namnjundu (319).

Yahya Kassim Issa

Jimbo la Chwaka mbunge wa jimbo hilo kwa miaka 20,  Yahya Kassim Issa aliangushwa baada ya kupata kura 1,572 dhidi ya mpinzani wake, Baguwanji Mensuriya Baguwanji aliyepata kura 1,951.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

SOCIALIZE

twitterfacebookgoogle plusemail

IN CASE YOU MISSED IT

FOR INSURANCE SERVICES CLICK HERE